Most searched:

Amirul Mu’minin (A.S) katika Kauli za Mtume Mtukufu (S.A.W.W)

Amirul Mu'minin (A.S) alikuwa na hadhi na daraja maalum mbele ya Mtume Mtukufu (S.A.W.W), na zimepokelewa kauli na hotuba nyingi kutoka kwa Mtume wa Mwisho kuhusu fadhila za Amirul Mu'minin.

Kuna kauli na maelezo mengi kutoka kwa Mtume Mtukufu (S.A.W.W) kuhusu fadhila za Amirul Mu’minin (A.S), ambapo baadhi yazo zinashughulikiwa katika makala hii.

Agizo la Mwenyezi Mungu Kuhusu Amirul Mu’minin (A.S)

Imepokelewa kutoka kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (S.A.W.W) akisema:

“Mwenyezi Mungu Mtukufu alinipa agizo kuhusu Ali (A.S). Nikasema: Ewe Mola wangu, nibainishie jambo hilo.

Akasema: Sikiliza. Nikasema: Ninasikiliza.

Akasema: ‘Ali (A.S) ni mshika bendera wa uwongofu, naye ni Imamu wa mawalii wangu, na ni nuru na mwangaza kwa kila anayetii amri zangu; yeye ndilo lile neno nililowausia wachamungu, atakayempenda amejitengenezea mapenzi nami, na atakayemfanyia uadui amefanya uadui nami.'” [1]

Kauli ya Mtume wa Mwisho Kuhusu Kufanana kwa Mzaliwa wa Kaaba na Manabii

Mtume wa Mwenyezi Mungu (S.A.W.W) amesema:

“Amirul Mu’minin Ali (A.S) katika mbingu ya saba ana nafasi kama ya jua linaloangaza mchana duniani, na katika mbingu ya dunia ana nafasi kama ya mwezi unaoangaza usiku duniani.

Mwenyezi Mungu amempa Ali (A.S) katika fadhila Zake kiasi kwamba sehemu ndogo tu inawatosha viumbe wote duniani, na Mungu amempa Ali (A.S) ufahamu na elimu kiasi kwamba kama ikigawanywa kwa watu wote duniani, kila mmoja atapata sehemu yake.

Huruma na upendo wake unafanana na huruma ya Luti, na maadili yake yanafanana na ya Yahya, zuhudi yake ni kama ya Ayubu, na ukarimu wake ni kama ukarimu wa Ibrahim, utukufu na haiba yake ni kama ya Suleiman bin Dawud, na nguvu zake ni kama nguvu za Dawud; yeye analo jina lililoandikwa kwenye milango yote ya peponi.” [2]

Njia Iliyonyooka na Haki Ziko Pale Aliposimama Ali

Imamu al-Baqir (A.S) akipokea kutoka kwa baba yake, na yeye kutoka kwa babu yake mtukufu amesema: “Mtume (S.A.W.W) amesema: Yeyote anayetaka kuvuka daraja la Sirati kwa wepesi na kuingia peponi bila hesabu, basi amwamini kiongozi (wilaya) wa wasii wangu, msaidizi wangu na makamu wangu, Ali bin Abi Talib (A.S). Na yeyote anayetaka kuingia katika moto wa Jahannam, basi aasi amri ya wilaya yake.

Naapa kwa utukufu na enzi ya Mwenyezi Mungu, hakika yeye ndiye ‘Babullah’ (Mlango wa Mungu) ambapo hakuna mtu anayeweza kumfikia Mungu isipokuwa kwa kupitia kwake; yeye ndiyo Njia Iliyonyooka ambayo Mungu atatuuliza kuhusu wilaya yake Siku ya Malipo.” [3]

Mtazamo Mwingine wa Pepo Kutoka kwa Mtume (S.A.W.W)

“Makhduj bin Yazid Al-Zuhli” alimwuliza Mtume (S.A.W.W):

“Ni nani watu wa peponi?” Hazrat akajibu: “Kila anayenitii mimi na kukubali wilaya ya Amirul Mu’minin Ali (A.S) baada yangu.”

Wakati huo Hazrat alishika mkono wa Amirul Mu’minin (A.S) na kusema: “Ali anatokana nami nami natokana na Ali. Atakayemfanyia uadui amefanya uadui nami, na atakayefanya uadui nami amemuasi Mungu na amesimama kupigana na Mungu.”

Kisha akasema: “Ewe Ali, vita nawe ni vita nami, na amani nawe ni amani nami. Wewe ndiyo ile bendera iliyoko kati yangu na umma wangu.” [4]

Ni Nani Imamu Aliyedhulumiwa?

Imepokelewa kutoka kwa “Ibn Abbas” kwamba Mtume (S.A.W.W) alisema: “Kama mtakuwa chini ya bendera ya wilaya ya Ali (A.S), hamtapotea kamwe wala hamtaangamia. Lakini mkienda kinyume naye, mtapotea upotevu mkubwa. Basi mcheni Mwenyezi Mungu, kwani yeye ndiye Imamu aliyedhulumiwa ambaye ameunganishwa na Mola.” [5]

Ushauri wa Mtume (S.A.W.W) Kuhusu Amirul Mu’minin (A.S) Katika Siku Zake za Mwisho

Mtume (S.A.W.W) alisema: “Enyi watu! Kifo changu kimekaribia, fahamuni kwamba nimebainisha hoja kwenu. Nawaachia kitabu cha Mungu na kizazi changu cha Ahlul-Bayt miongoni mwenu.”

Wakati huo Mtume alishika mkono wa Amirul Mu’minin (A.S) na kusema: «عَلِی مَعَ الْقُرْآنِ وَ الْقُرْآنُ مَعَ عَلِی» (Ali yuko na Kurani na Kurani iko na Ali), hawatatengana kamwe hadi watakaporejea kwangu kwenye Hodhi ya Kawthar, nami nitawauliza kuhusu yale yaliyotokea baada yangu.” [6]

Ni Lini Ali (A.S) Alipewa Lakabu ya “Amirul Mu’minin”?

Imepokelewa kutoka kwa “Huzaifa” kwamba Mtume (S.A.W.W) alisema: “Kama watu wangejua ni lini Ali (A.S) alipewa lakabu ya Amirul Mu’minin, wasingewahi kusahau fadhila na utukufu wake.

Amirul Mu’minin na Adamu wote waliitwa kwa jina hili tangu walipokuwa kati ya maji na udongo.

Wakati ule Mwenyezi Mungu Mtukufu aliposema: Je, Mimi siye Mola wenu?

Wakasema: Ndiyo. Mwenyezi Mungu Mtukufu akasema: Mimi ndiye Mola wenu, Muhammad ni Mtume wenu, na Ali ni kiongozi na amiri wenu.” [7]

Ushufaaji wa Mtume (S.A.W.W) Hautawafikia Watu Gani?

Imepokelewa kutoka kwa Ibn Abbas kwamba Mtume (S.A.W.W) alisema: “Yeyote anayetaka kuishi na kufa kama nilivyoishi na kufa mimi, na kuingia katika pepo tukufu ya Mungu, basi amfuate Ali (A.S) baada yangu, awe mshikaji wa njia ya Ali (A.S), na afuate Ahlul-Bayt wangu ambao ni kizazi cha damu yangu na wamepata sehemu ya elimu na ujuzi wangu.

Ole wao wasio na imani na wenye kukataa katika umma wangu, ambao watabaki katika adhabu ya upotevu; watu hawa sina uhusiano wala urafiki nao, na shufaa yangu haitawafikia kamwe.” [8]

Sharti la Imani ya Kweli kwa Mtume (S.A.W.W)

Mtume (S.A.W.W) alisema: “Ewe Mola wangu, kila anayeniamini mimi, basi ni lazima akubali wilaya ya Ali bin Abi Talib (A.S), kwani wilaya yake ni wilaya yangu, na wilaya yangu ni wilaya ya Mwenyezi Mungu.” [9]

Mtume (S.A.W.W) alisema: “Yeyote anayetaka maisha na kifo chake viwe kama vyangu, na aingie peponi, basi anyenyekee mbele ya wilaya ya Ali (A.S) na kizazi chake.” [10]

Ni Nini Kilichomliza Mtume (S.A.W.W) Alipomwona Amirul Mu’minin (A.S)?

Imepokelewa kutoka kwa Ibn Abbas: “Mtume wa Mwenyezi Mungu (S.A.W.W) alikuwa ameketi sehemu fulani, ghafla Amirul Mu’minin (A.S) akafika njiani.

Mtume (S.A.W.W) alipomwona alilia na kusema: ‘Njoo karibu nami.. njoo.. ewe ndugu yangu…’

Amirul Mu’minin (A.S) alimkaribia hadi akaketi upande wa kulia wa Mtume, na wakati huo Mtume wa Mwenyezi Mungu (S.A.W.W) alisema: ‘Yeye ni ndugu yangu na sehemu ya mwili wangu. Yeye ndiye mwenye mamlaka na mshika bendera wangu duniani na Akhera. Yeye ndiye mmiliki wa Hodhi ya Kawthar na mtoa shufaa wangu.

Yeye ni kiongozi na mola wa kila Mwislamu. Yeye ni Imamu wa kila muumini na kiongozi wa kila mwenye moyo msafi, naye ni wasii wangu na makamu wangu kwa familia yangu na umma wangu, sasa na baada yangu. Wanaompenda ni wapendwa wangu, na maadui zake ni maadui zangu.

Kwa kupitia wilaya yake, rehema ya Mwenyezi Mungu imeenea katika umma wangu, na kwa sababu ya kwenda kinyume naye, watu wanakabiliwa na laana na ghadhabu ya Mungu. Nilipomwona Ali nililia, kwa sababu niliona usaliti ambao umma huu utamfanyia, hadi kufikia hatua ya kumwondoa katika ukhalifa wangu.

Mwenyezi Mungu amemweka kama mbadala wangu, atakuwa makamu wangu hadi atakapopigwa jeraha kwenye kichwa chake kitukufu, litakalolaza uso na ndevu zake takatifu kwa damu, katika kipindi ambacho ni mwezi bora zaidi mbele ya Mungu, yaani mwezi mtukufu wa Ramadhani ambao Qurani ilishuka ndani yake ili iwe uwongofu, mwangaza na ukombozi kwa walimwengu.'” [11]

Kueleza Fadhila za Amirul Mu’minin (A.S) kwa Mtume (S.A.W.W) Wakati wa Miiraj

Mtume wa Mwenyezi Mungu (S.A.W.W) alisema: “Wakati nilipopelekwa Miiraj mbinguni hadi juu ya ‘Sidratul Muntaha’, nilisimama mbele ya Mwenyezi Mungu Azza wa Jalla, na Mungu akaniita akisema: Ewe Muhammad!

Nikasem: Labbaika ya Allah.

Akasema: Umewajaribu waja wangu wote, ni nani kati yao aliye mcha Mungu zaidi na mwenye kukutii zaidi? Nikasema: Ewe Mola wangu! Ali.

Akasema: Umesema kweli ewe Muhammad.

Je, umemchagua mbadala wako baada yako ambaye ataendeleza utume wako na kuwafundisha waja wangu kitabu changu?

Nikasema: Hapana, Wewe nichagulie, kwani chaguo Lako ndilo bora zaidi.

Akasema: Nimekuchagulia Ali, basi mweke kuwa wasii na makamu wako, kwani nimempa elimu na ustahimilivu wangu; hakika yeye ndiye ‘Amirul Muminina’ ambaye hakuna kiongozi aliyekuwa kabla yake wala hatakuwapo baada yake.

Ewe Muhammad, Ali ni mshika bendera wa uwongofu. Yeye ni Imamu wa waja wangu na nuru ya mawalii wangu. Yeye ndilo lile neno nililowaitia wachamungu kwalo. Atakayempenda amejitengenezea mapenzi nami, na atakayemfanyia uadui amefanya uadui nami, basi mpe habari njema hii, ewe Muhammad.” [12]

Onyo la Mtume (S.A.W.W) Kuhusu Kutokea kwa Fitna Katika Siku Zake za Mwisho

Mtume (S.A.W.W) alisema: “Baada yangu itatokea fitna. Katika fitna hiyo mfuateni Ali bin Abi Talib (A.S). Yeye ndiye mtu wa kwanza atakayeniona Siku ya Kiyama na kuweka mkono wake kwenye mkono wangu. Yeye ndiye yule mkweli mkuu na mmulikaji wa umma huu anayetenganisha haki na batili, naye ndiye Ya’asubul Muminina (kiongozi wa waumini).” [13]

Maelezo ya Chini

[1] Al-Amali, Sheikh Al-Saduq: uk 565.

[2] Al-Amali, Sheikh Al-Saduq: uk 57.

[3] Bihar al-Anwar, Allamah Majlisi: Jz 38, uk 98.

[4] Yanabi’ul Mawaddah, Hafiz Al-Qanduzi: Jz 1, uk 65.

[5] Yanabi’ul Mawaddah, Hafiz Al-Qanduzi: Jz 2, uk 293.

[6] Al-Amali, Al-Tusi: uk 478.

[7] Ihkakul Haqq wa Izhaqul Batil, Al-Tustari: Jz 15, uk 227.

[8] Fara’idus Simtain, Al-Hamawini Al-Shafi’i: Jz 1, uk 64.

[9] Al-Amali, Sheikh Al-Tusi: Jz 1, uk 812.

[10] Al-Manaqib, Al-Khwarazmi: Jz 1, uk 76.

[11] Fara’idus Simtain, Al-Hamawini Al-Shafi’i: Jz 2, uk 25.

[12] Fara’idus Simtain, Al-Hamawini Al-Shafi’i: Jz 1, uk 244.

[13] Yanabi’ul Mawaddah, Hafiz Al-Qanduzi, Jz 1, uk 154.

Yaliyomo zaidi

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *