Most searched:

Muhammad bin Abi Bakr, Gavana Shujaa wa Amirul Muuminiin (amani iwe juu yake) katika Ardhi ya Misri

“Muhammad bin Abi Bakr” alikuwa mwana wa Abu Bakr aliyekulia na kulelewa katika nyumba ya Amirul Muuminiin (amani iwe juu yake). Muhammad alikuwa miongoni mwa masahaba waaminifu na wenye kutegemewa wa Amirul Muuminiin (amani iwe juu yake), naye aliteuliwa na Imam kuwa gavana wa Misri. Aliuwawa shahidi wakati wa uvamizi wa majeshi ya Sham dhidi ya Misri.

Muhammad bin Abi Bakr, aliyepewa lakabu ya Mwabudu wa Maquraish, alikuwa mwana wa Abu Bakr, khalifa wa kwanza, na alikuwa miongoni mwa masahaba na Mashia maalumu wa Amirul Muuminiin (amani iwe juu yake). Kulikuwa na upendo wa pande mbili kati yake na Imam, na Imam alikuwa akimwita mwanawe. Pia alikuwa miongoni mwa wapinzani mashuhuri wa utendaji wa khalifa wa tatu. Hatimaye, tarehe 14 ya mwezi wa Swafar mwaka 38 Hijria, aliuwawa shahidi na jeshi la Muawiya.

Chini ya Malezi ya Bwana wa Wachamungu

Muhammad bin Abi Bakr alikuwa mwana wa khalifa wa kwanza na Asmaa bint Umais. Baada ya kufariki kwa Abu Bakr na kuolewa kwa Asmaa na Amirul Muuminiin (amani iwe juu yake), Muhammad alikulia na kulelewa katika nyumba ya Amirul Muuminiin (amani iwe juu yake). Fiqhi, maarifa na fikra zake zilitokana na mafundisho safi ya Bwana wa Wachamungu. Hakumtambua mtu yeyote, hata baba yake Abu Bakr, kuwa na fadhila sawa na za Amirul Muuminiin (amani iwe juu yake). Bali wakati wa kuweka kiapo cha uaminifu kwake alisema: “Ninashuhudia kwamba wewe ni Imam ambaye ni wajibu kutiiwa.”

Amirul Muuminiin (amani iwe juu yake) pia alimpenda na alimhesabu kuwa “mwanawe kutoka katika uti wa mgongo wa Abu Bakr.” Katika Nahjul Balagha imenukuliwa kutoka kwake: “Yeye, Muhammad, alikuwa kipenzi changu, nami nilimlea kama mwanangu.” [1]

Alikuwa miongoni mwa makamanda wa jeshi la Amirul Muuminiin (amani iwe juu yake) katika vita vya Jamal na Swiffin. Muhammad aliteuliwa na Imam kuwa gavana wa Misri.

Kuweka Kiapo cha Uaminifu kwa Amirul Muuminiin (amani iwe juu yake)

Imam Swadiq (amani iwe juu yake), alipomtaja Muhammad bin Abi Bakr, alisisitiza kiapo chake kipya na cha dhati cha uaminifu kwa Amirul Muuminiin (amani iwe juu yake); kiapo ambacho ndani yake alishuhudia kwa unyenyekevu kwamba Imam ni kiongozi ambaye ni wajibu kutiiwa.

Hamza bin Muhammad al-Tayyar, aliyekuwa miongoni mwa wapokezi wa kuaminika wa Imam Swadiq (amani iwe juu yake), anasimulia kwamba Muhammad bin Abi Bakr alitajwa mbele ya Imam. Imam akasema: “Mwenyezi Mungu amrehemu na amteremshie rehema; siku moja alimwambia Amirul Muuminiin (amani iwe juu yake): ‘Nyoosha mikono yako ili niweke kiapo cha uaminifu kwako.’ Imam akasema: ‘Je, hujafanya hivyo?’ Akasema: ‘Ndiyo.’ Basi Imam akanyoosha mkono wake, naye Muhammad akasema: ‘Ninashuhudia kwamba wewe ni Imam ambaye ni wajibu kutiiwa.’”

Kisha Imam Swadiq (amani iwe juu yake) akasema: “Uungwana na heshima ya Muhammad bin Abi Bakr vilimfikia kupitia mama yake, Asmaa bint Umais, si kupitia baba yake.” [2]

Katika sehemu nyingine, Zurara, aliyekuwa miongoni mwa masahaba wa Imam Baqir na Imam Swadiq (amani iwe juu yao), anasema kwamba Imam Baqir (amani iwe juu yake) alisema: “Muhammad bin Abi Bakr aliweka kiapo cha uaminifu kwa Amirul Muuminiin (amani iwe juu yake) baada ya kujitenga na baba yake.” [3]

Barua kwa Muawiya katika Kumtetea Bwana wa Wachamungu

Muhammad bin Abi Bakr, kama Bwana wake Amirul Muuminiin (amani iwe juu yake), alimwona Muawiya kuwa mnyakuzi wa haki, dhalimu na mdanganyifu. Kwa sababu hiyo, katika siku za mwanzo za utawala wake nchini Misri, alimwandikia Muawiya barua ambamo alimweleza Amirul Muuminiin (amani iwe juu yake) kuwa ndiye mtu pekee anayestahili Uimamu na Ukhalifa.

Muhammad bin Abi Bakr alimwandikia Muawiya bin Abi Sufyan:

“Mwenyezi Mungu, kwa utukufu, ukuu, mamlaka na uwezo Wake juu ya viumbe Vyake vyote, na kwa ubora wa hoja Zake, aliwaumba viumbe si kwa mchezo, udhaifu wala uhitaji, bali aliwaumba ili wamwabudu. Akawafanya baadhi wapotovu, baadhi waongofu, kundi moja lenye mashaka na jingine lenye saada. Kisha, kwa elimu Yake, akamchagua Mtume wa Mwenyezi Mungu (rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na Aali zake), akamteua kwa ukaribu Wake, akamchagua kwa mapenzi Yake, na akamtuma akiwa mwaminifu wa ujumbe Wake. Akamtuma kwa wahyi Wake na akamtegemea katika jambo Lake kama Mtume mkweli, mwenye kuongoza, mwonyeshaji wa njia, mtoaji wa bishara na mwonyaji.

Mtu wa kwanza kuitikia wito wake, kumsadiki, kumwamini na kudhihirisha Uislamu alikuwa ndugu yake, binamu yake, wasii wake, mrithi wa elimu yake na khalifa baada yake; yule ambaye Mtume wa Mwenyezi Mungu (rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na Aali zake), kwa amri ya Mwenyezi Mungu, alimteua kuwa mrithi wake; yaani Amirul Muuminiin Ali bin Abi Talib (amani iwe juu yake). Aliyasadiki mambo ya siri ya Mtume (rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na Aali zake), na Mtume alikuwa akimfadhilisha kuliko jamaa zake wa karibu zaidi. Alimlinda dhidi ya kila hatari, alimsaidia katika kila tukio la kutisha, alipigana na yeyote ambaye Mtume alipigana naye, na alifanya amani na yeyote ambaye Mtume alifanya amani naye. Amirul Muuminiin (amani iwe juu yake) daima aliutoa uhai wake mbele ya Mtume (rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na Aali zake) katika nyakati za hofu, njaa na shida, hadi Mwenyezi Mungu Mtukufu alipouweka wazi wito wake na kukamilisha hoja yake.

Ewe Muawiya! Wewe uliye mpotovu, unajifaharisha mbele yake? Ilhali yeye ni mtu msafi na mtangulizi zaidi wa Umma huu. Yeye ndiye mwadilifu zaidi, mwenye sifa bora zaidi, mwenye mke aliyebobea zaidi na mwenye daraja ya juu zaidi. Wakati wa Hijra ya Mtume (rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na Aali zake), alitoa roho yake ili kumwokoa kutoka mikononi mwa maadui zake, akalala katika kitanda chake, na akauza nafsi yake kwa Mwenyezi Mungu kwa ajili ya kumwokoa Mtume (rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na Aali zake).

Ami yake, Hamza, alikuwa bwana wa mashahidi wa vita vya Uhud, na baba yake alikuwa mtetezi wa Mtume (rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na Aali zake) dhidi ya maadui wa Mwenyezi Mungu. Lakini wewe na baba yako mliendelea kuwachochea, na kwa kutumia mali mlihamasisha makabila ya Waarabu ili kuuzima nuru ya Mwenyezi Mungu. Baba yako alikufa akiwa katika mwenendo huo, na wewe ukawa mrithi wake. Ushahidi wa matendo yako hayo ni kuja kwako na kutafuta hifadhi kwako kwa masalia ya makundi ya ushirikina, viongozi wa unafiki, na maadui wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na Aali zake) pamoja na Ahlul Baiti wake.

Kwa upande mwingine, ushahidi wa fadhila zilizo wazi za Amirul Muuminiin (amani iwe juu yake) na kutangulia kwake kwa muda mrefu katika Uislamu ni wafuasi wake; wale ambao Mwenyezi Mungu Mtukufu amewataja pamoja na fadhila zao katika Qurani Tukufu, na amewasifu Muhajirina na Ansar. Makundi miongoni mwao, wanaotembea kwa miguu na wanaopanda, wapo pamoja naye. Wanapigana kwa panga zao, wanamwaga damu zao katika kumtetea, wanaona saada katika kumtii na mashaka katika kuikhalifu amri yake.

Ole wako! Na tena ole wako! Unawezaje kujilinganisha na Ali? Yeye ni ndugu wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na Aali zake), baba wa watoto wake na mshirika wake katika mambo yote, ilhali wewe ni adui wa Mtume wa Mwenyezi Mungu na mwana wa adui yake. Basi furahia batili yako, kwa sababu mwana wa Aas anakuingiza zaidi katika kina cha upotovu wako. Ni kana kwamba muda wako umekaribia kwisha na hila pamoja na ujanja wako vimedhoofika. Tambua kwamba umemfanyia Mola wako hila kwa kujiona salama dhidi ya mpango Wake. Umejiweka mbali na rehema ya Mwenyezi Mungu, na sasa Mwenyezi Mungu anakuvizia, ilhali bado uko katika kiburi na ukaidi dhidi Yake. Sisi, kwa msaada wa Mwenyezi Mungu, Mtume Wake na Ahlul Baiti wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na Aali zake), hatukuhitaji.” [4]

Namna Alivyouwawa Shahidi

Muawiya, kwa lengo la kulipiza kisasi na kuiteka Misri, kupitia Amr bin Aas na kwa ushirikiano wa waasi, alimtuhumu Muhammad kwa kuhusika katika mauaji ya Uthman na akamshambulia. Muhammad alipokea amri ya kusimama imara kutoka kwa Amirul Muuminiin (amani iwe juu yake) na akapambana. Hata hivyo, baada ya shahada ya Malik al-Ashtar, jeshi lake lilishindwa mbele ya wanajeshi 6000 wa Sham katika eneo la al-Masannat.

Baada ya jeshi la Muhammad kushindwa na watu wa Sham, wale waliokuwa karibu naye walimwacha peke yake na kukimbia. Mwishowe alikimbilia katika magofu, ambako Muawiya bin Hudayj alimuua shahidi na kisha akamchoma moto. [5]

Katika Maombolezi ya Muhammad bin Abi Bakr

Amirul Muuminiin (amani iwe juu yake), kwa kueleza nafasi ya kina ya Muhammad bin Abi Bakr na uhusiano wao wa kifamilia, alizungumza kuhusu uchungu wa shahada yake na juhudi alizofanya kuzuia matukio ya Misri.

Habari ya shahada ya Muhammad bin Abi Bakr ilipomfikia Amirul Muuminiin (amani iwe juu yake), Imam alisema: “Huzuni yetu kwa shahada yake ni sawa na furaha ya watu wa Sham; tofauti ni kwamba adui mmoja amepungua kutoka kwao, na rafiki mmoja amepungua kutoka kwetu.” [6]

Malik bin Jaun al-Hadhrami anasimulia kutoka kwa wapokezi kwamba Amirul Muuminiin (amani iwe juu yake) alisema kuhusu Muhammad: “Mwenyezi Mungu amrehemu Muhammad bin Abi Bakr. Alikuwa kijana mwenye umri mdogo. Naapa kwa Mwenyezi Mungu, nilikuwa nimekusudia kumteua Hashim bin Utba, maarufu kwa lakabu ya Mirqal, kuwa gavana wa Misri. Naapa kwa Mwenyezi Mungu, lau yeye angekuwa gavana wa Misri, angeifunga njia dhidi ya Amr bin Aas na wafuasi wake, na asingeliuwawa isipokuwa akiwa na upanga wake mkononi.”

Kisha Imam, akisisitiza kwamba kauli hiyo haikumaanisha kumlaumu Muhammad bin Abi Bakr, akaongeza: “Alitumia uwezo wake wote na akatekeleza wajibu wake kikamilifu.”

Amirul Muuminiin (amani iwe juu yake) akaulizwa: “Ewe Amirul Muuminiin! Kwa nini umehuzunika sana kwa shahada yake?”

Imam akasema: “Kwa nini nisihuzunike?! Alilelewa katika malezi yangu; kwa watoto wangu alikuwa kama ndugu yao, nami nilikuwa kama baba yake na nilimhesabu kuwa kama mwanangu.” [7]

Nafasi ya Muhammad bin Abi Bakr mbele ya Bwana wa Wachamungu

Amirul Muuminiin (amani iwe juu yake), katika barua aliyomwandikia Ibn Abbas, huku akiomboleza shahada ya Muhammad bin Abi Bakr, alisisitiza sifa zake za kimaadili na akalalamikia kutojali na udhaifu wa watu katika kumsaidia mtumishi huyo mwaminifu.

Alimwandikia Ibn Abbas:

“Kwa hakika Misri imeanguka, na gavana wake Muhammad bin Abi Bakr, ambaye Mwenyezi Mungu amrehemu, ameuwawa shahidi. Mbele ya Mwenyezi Mungu tunamhesabu kuwa mwana mwenye kunasihi kwa dhati, mtumishi mwenye bidii, upanga mkali na nguzo ya kuzuia maadui. Daima niliwaita watu wajiunge naye na nikawaamuru waharakishe kumsaidia kabla ya kutokea kwa matukio haya mabaya. Niliwaita watu kwa siri na kwa wazi, tangu mwanzo hadi mwisho. Baadhi walikuja kwa kulazimishwa, wengine walitoa visingizio vya uongo, na wengine walibaki kwa unyonge na udhalili. Ninamuomba Mwenyezi Mungu aniokoe hivi karibuni kutoka miongoni mwa watu hawa. Naapa kwa Mwenyezi Mungu, lau si tamanio langu la kuuwawa shahidi katika kupigana na adui, na lau singelikuwa nimejiandaa kwa kifo, nisingependa kukaa pamoja na watu hawa hata kwa siku moja wala kukutana nao.” [8]

Vyanzo

[1] Sayyid Radi, Nahjul Balagha, Hotuba ya 67, tafsiri ya Muhammad Dashti, Qum, Machapisho ya Mashhur, 1380 Hijria Shamsia.
[2] Bihar al-Anwar, Juzuu ya 33, ukurasa wa 582.
[3] Bihar al-Anwar, Juzuu ya 33, ukurasa wa 585.
[4] Waq’at al-Jamal, Juzuu ya 1, ukurasa wa 89.
[5] Ibn Shabba, Umar bin Shabba, Tarikh Madinat al-Munawwara, Juzuu ya 4, ukurasa wa 1285.
[6] Bihar al-Anwar, Juzuu ya 33, ukurasa wa 590; Nahjul Balagha, Juzuu ya 1, ukurasa wa 532.
[7] Bihar al-Anwar, Juzuu ya 33, ukurasa wa 566.[8] Bihar al-Anwar, Juzuu ya 33, ukurasa wa 592.

Yaliyomo zaidi

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *