Roho tukufu ya Mtume wa Uislamu (rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie yeye na Aali zake) ilipaa kuelekea kwa Mola katika siku ya 28 ya Safar, akiwa mikononi mwa Amirul Muuminiin (amani iwe juu yake). Baada ya shahada yake, wakati viongozi wa Muhajirina na Ansari walipokuwa wakibishana katika Saqifa ya Bani Saa’ida kuhusu mrithi wake, Amirul Muuminiin (amani iwe juu yake) alishughulika na kuuosha na kuuvisha sanda mwili wa Mtume wa Mwisho (rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie yeye na Aali zake).
Wasia wa Mwisho kwa Bwana wa Wachamungu
Katika usiku wa mwisho wa maisha ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie yeye na Aali zake), alimwomba Amirul Muuminiin (amani iwe juu yake) alete karatasi, kisha akamwandikishia wasia huu ambao ndani yake aliwatambulisha warithi wake baada yake.
Amirul Muuminiin Imam Ali (amani iwe juu yake) anasimulia kwamba katika usiku wa shahada ya Mtume (rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie yeye na Aali zake), aliniambia: “Ewe Abal Hassan! Leta kalamu na karatasi.” Kisha Mtume wa Mwenyezi Mungu (rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie yeye na Aali zake) aliniandikishia maandishi ya wasia wake, nami nikaandika. Alipofika katika sehemu hii alisema: “Ewe Ali! Baada yangu watakuja Maimamu kumi na wawili, na wewe ndiye wa kwanza wao. Mwenyezi Mungu amekuita mbinguni kwa majina haya: Ali Murtadha, Amirul Muuminiin, Siddiq al-Akbar, Faruq al-A’dham, Ma’mun na Mahdi; na hakuna yeyote isipokuwa wewe anayestahili majina haya.
Ewe Ali! Baada yangu, wewe ndiye wasii wangu juu ya watu wa nyumba yangu, walio hai na waliokufa, na juu ya wake zangu. Yeyote katika wake zangu utakayemweka, atakutana nami Siku ya Kiyama, na yeyote utakayempa talaka, mimi nimejitenga naye; yeye hataniona wala mimi sitamwona katika uwanja wa Kiyama. Pia wewe ndiye Khalifa na mrithi wangu juu ya Umma wangu.
Wakati wa kufariki kwako utakapofika, mkabidhi ukhalifa mwanangu Imam Hassan, kwani yeye ni mwema na mwenye kuunganisha. Baada yake, akabidhi ukhalifa kwa mwanangu Imam Hussein, shahidi huyo mtakatifu atakaye uwawa. Wakati wa kufariki kwa Imam Hussein utakapofika, amkabidhi mwanaye Imam Ali, Sayyid al-Abidin na mwenye alama za kusujudu. Kisha yeye amkabidhi mwanaye Imam Muhammad, Baqir al-Ilm, naye amkabidhi mwanaye Imam Ja’far Sadiq. Baada yake, kwa mwanaye Imam Musa bin Ja’far al-Kadhim, kisha kwa mwanaye Imam Ali al-Ridhaa, kisha kwa mwanaye Imam Muhammad Taqi, na baada yake kwa mwanaye Imam Ali Nasih. Kisha naye amkabidhi mwanaye Imam Hassan Fadhil, na mwishowe yeye ataukabidhi ukhalifa kwa mwanaye Imam Muhammad, ambaye ndiye akiba ya Aali Muhammad (rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie yeye na Aali zake). Hao ndio Maimamu kumi na wawili ambao ni warithi wangu.”[1]
Kutabiriwa kwa Shahada ya Familia ya Utume
Mtume Mtukufu (rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie yeye na Aali zake), katika siku za mwisho za maisha yake, alieleza hatima ya shahada iliyokuwa imekadiriwa kwake na kwa Ahlul Baiti wake watukufu.
Mtume wa Mwenyezi Mungu (rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie yeye na Aali zake) alisema: “Hakuna yeyote miongoni mwetu isipokuwa atalishwa sumu au atauawa.”[2]
Amirul Muuminiin Imam Ali bin Abi Talib (amani iwe juu yake) alisimama huku akitokwa na machozi na kusema: “Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu! Baba yangu na mama yangu wawe fidia yako! Je, wewe pia utauawa?” Mtume (rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie yeye na Aali zake) akajibu: “Ndiyo! Nitalishwa sumu na nitapata shahada. Wewe utauawa kwa upanga na ndevu zako zitapakwa damu ya kichwa chako. Mwanangu Imam Hassan atapata shahada kwa sumu, na mwanangu Imam Hussein atauawa kwa upanga; atauawa na mwana wa dhalimu ambaye ni dhalimu, mwana wa najisi ambaye ni najisi, mwana wa mnafiki ambaye ni mnafiki.”[3]
Mkutano wa Mwisho
Katika saa za mwisho za maisha ya Mtume (rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie yeye na Aali zake), Amirul Muuminiin (amani iwe juu yake) ndiye pekee aliyepata heshima ya kuwa faraghani na kufanya mazungumzo ya siri naye.
Ummu Salama anasema: “Naapa kwa Mwenyezi Mungu ambaye Ummu Salama huapa kwa jina Lake, mtu wa mwisho aliyekutana na kuwa pamoja na Mtume wa Mwenyezi Mungu (rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie yeye na Aali zake) alikuwa Amirul Muuminiin (amani iwe juu yake). Asubuhi ya siku ambayo Mtume wa Mwenyezi Mungu alifariki, alikuwa amemtuma Imam Ali kutekeleza jambo fulani. Aliendelea kusema: ‘Je, Ali amefika?’ na alirudia kauli hii mara tatu. Hatimaye, Imam Ali bin Abi Talib (amani iwe juu yake) aliwasili kabla ya kuchomoza kwa jua. Tulipogundua kwamba Mtume wa Mwenyezi Mungu (rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie yeye na Aali zake) alikuwa na jambo la faragha naye, tukatoka chumbani. Amirul Muuminiin (amani iwe juu yake) akainama karibu na kitanda cha Mtume (rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie yeye na Aali zake), na ndiye aliyekuwa mtu wa mwisho kuwa naye faraghani; kisha Mtume (rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie yeye na Aali zake) akazungumza naye kwa sauti ya chini na kumnong’oneza.”[4]
Dakika za Kuhuzunisha za Shahada
Amirul Muuminiin Imam Ali (amani iwe juu yake), katika Khutba ya 197 ya Nahjul Balagha, anaelezea dakika za mwisho za maisha matukufu ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie yeye na Aali zake) kwa maneno haya: “Roho ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie yeye na Aali zake) ilichukuliwa huku kichwa chake kikiwa juu ya kifua changu, na pumzi yake ya mwisho ikapita mikononi mwangu. Kisha nikaipaka usoni mwangu. Mimi ndiye niliyesimamia kumuosha, huku Malaika wakinisaidia. Mlango, kuta na Sahni ya nyumba vilijaa vilio. Kundi moja [la Malaika] lilikuwa likishuka ardhini na kundi jingine likipanda mbinguni, na masikio yangu hayakuacha kusikia sauti zao wakimswalia kwa sauti ya chini, hadi tulipomzika kaburini. Ni nani anayestahiki kuwa karibu naye katika uhai na kifo chake kuliko mimi?”
Mazishi ya Mtume wa Mwisho
Shahada ya Mtume (rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie yeye na Aali zake) ilikuwa mwanzo wa maombolezi makubwa ya masahaba na wafuasi wake katikati ya huzuni na majonzi. Katika hali hiyo, Bwana wa Wachamungu, kwa busara na kwa ushirikiano wa watu wake wa karibu, aliandaa taratibu za kumuaga na kumzika Mjumbe wa Mwisho wa Mwenyezi Mungu.
Mtume (rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie yeye na Aali zake) alifariki akiwa mikononi mwa Amirul Muuminiin (amani iwe juu yake), na Imam Ali alimwosha akiwa bado na nguo yake kwa msaada wa Fadhl bin Abbas, Usama bin Zaid na wengine, kisha wakamvisha sanda. Kwa pendekezo la Bwana wa Wachamungu, watu waliingia nyumbani kwa Mtume kwa makundi na kumswalia bila kumfuata mtu yeyote kama Imam, na utaratibu huo uliendelea hadi siku iliyofuata.[5] [6]
Kwa mujibu wa baadhi ya riwaya, kulikuwa na mapendekezo mbalimbali kuhusu mahali pa kumzika Mtume (rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie yeye na Aali zake), lakini Amirul Muuminiin (amani iwe juu yake) alisisitiza kwamba Mwenyezi Mungu huchukua roho za Manabii katika maeneo yaliyo safi zaidi. Wote walikubaliana, na mwili wa Mtume (rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie yeye na Aali zake) ukazikwa katika sehemu ileile aliyofariki. Abu Ubaida Jarrah na Zaid bin Sahl waliandaa kaburi, na Amirul Muuminiin (amani iwe juu yake), kwa msaada wa Fadhl bin Abbas na Usama bin Zaid, aliuzika mwili wa Mtume (rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie yeye na Aali zake).[7]
Tukio la Saqifa na Mtihani wa Mwenyezi Mungu
Baada ya shahada ya Mtume (rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie yeye na Aali zake), wakati Amirul Muuminiin (amani iwe juu yake) alikuwa akishughulika na mazishi yake, baadhi ya Masahaba walikusanyika Saqifa na kujadiliana kuhusu ukhalifa na urithi wa uongozi.
Baada ya suala la [kunyang’anywa] ukhalifa wa Abu Bakr kukamilika na watu kuweka kiapo cha uaminifu kwake, mtu mmoja alimjia Amirul Muuminiin (amani iwe juu yake), wakati Imam alikuwa akimwaga udongo juu ya kaburi la Mtume (rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie yeye na Aali zake) huku akiwa ameshika koleo. Mtu huyo alisema: “Watu wameweka kiapo cha uaminifu kwa Abu Bakr, Ansari wamepatwa na udhalili na unyonge, na Tulaqa’ — wale ambao Mtume aliwaacha huru katika ushindi wa Makka — wameharakia kuweka kiapo cha uaminifu kwa Abu Bakr ili cheo hiki kisije kikakufikia wewe!”
Amirul Muuminiin (amani iwe juu yake) aliposikia habari hiyo, alishika mpini wa koleo na kuuchoma ardhini, kisha akasoma aya ya 1 hadi ya 4 za Suratul Ankabut:
« بِسمِ اللهِ الرَّحمٰنِ الرَّحیمِ، الم، أ حَسِبَ النّاسُ أن یُترَکوا أن یَقولوا آمَنّا و هُم لا یُفتَنونَ، و لَقَد فَتَنّا الَّذینَ مِن قَبلِهِم فَلَیَعلَمَنَّ اللهُ الَّذینَ صَدَقوا و لَیَعلَمَنَّ الکاذِبینَ، أم حَسِبَ الَّذینَ یَعمَلونَ السَّیِّئاتِ أن یَسبِقونا ساءَ ما یَحکُمونَ،
“Kwa jina la Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema, Mwenye Kurehemu. Alif Laam Miim. Je, watu wanadhani kwamba wataachwa kwa kusema tu: ‘Tumeamini,’ bila kujaribiwa? Hakika tuliwajaribu wale waliokuwa kabla yao, ili Mwenyezi Mungu awabainishe wale waliosema kweli na awabainishe waongo. Au wale wanaofanya maovu wanadhani kwamba watatuepuka? Ni uamuzi mbaya ulioje wanaoutoa.”[8]
Vyanzo
[1] Al-Ghayba ya al-Tusi, Juzuu ya 1, ukurasa wa 150.
[2] Kifayat al-Athar, Juzuu ya 1, ukurasa wa 226; Bihar al-Anwar, Juzuu ya 27, ukurasa wa 216; Bihar al-Anwar, Juzuu ya 43, ukurasa wa 363; Ithbat al-Hudat, Juzuu ya 1, ukurasa wa 344.
[3] Kitab Sulaim, Juzuu ya 2, ukurasa wa 834.
[4] Bihar al-Anwar, Juzuu ya 22, ukurasa wa 472.
[5] Sheikh Mufid, al-Irshad, 1413 H, Juzuu ya 1, ukurasa wa 188.
[6] Ya’qubi, Tarikh al-Ya’qubi, Dar Sadir, Juzuu ya 2, ukurasa wa 114.
[7] al-Irbili, Kashf al-Ghumma, 1381 H, Juzuu ya 1, ukurasa wa 19.
[8] Bihar al-Anwar, Juzuu ya 24, ukurasa wa 230.