Most searched:

Ghadhabu ya Amirul Muuminina (amani iwe juu yake) kwa Woga na Ulegevu wa Watu wa Kufa

Amirul Muuminina (amani iwe juu yake) alitoa hotuba ya 34 ya Nahjul Balagha kuhusu kuhamasisha watu wa Kufa kwenda kupigana na watu wa Shamu. Katika hotuba hii, kwanza anawakemea watu kwa sababu ya ulegevu na kutojali kwao kuhusu jihadi na wajibu wa kidini, na kisha anafafanua haki za pande zote mbili kati ya kiongozi na watu; haki ambazo watu wanazo juu ya mtawala na haki ambazo mtawala anazo juu ya watu.

Imamu (amani iwe juu yake) alisema:

“Nimechoka kuwakemea. Laana iwe juu yenu! Nimechoka kwa kiasi  nilivyowakemea ninyi!

Je, mmeridhika na maisha ya muda ya dunia badala ya maisha ya akhera? Na mmechagua taabu na udhalilifu badala ya utukufu na heshima?

Kila ninapowaita kwenye jihadi dhidi ya adui, macho yenu yanazunguka kwenye mboni zake kwa uwoga, kana kwamba uwoga wa kifo umewanyanya akili zenu na mmepoteza fahamu na kuchanganyikiwa kama walevi wasioweza kujibu, na kana kwamba mmepoteza akili zenu na hamfahamu. Mimi kamwe na hata siku moja siwaamini ninyi, hakuna tegemeo kwenu la kuegemea (katika kumfukuza adui), na wala ninyi si kabila au wasaidizi wenye heshima wa kunyoosha mkono wa shida kwenu. Mko kama ngamia wasio na mchungaji ambao kila wanapokusanyika upande mmoja, hutawanyika upande mwingine.

Naapa kwa Mwenyezi Mungu! Ninyi ni chombo kibaya cha kuwasha moto wa vita dhidi ya maadui, wanapanga mikakati dhidi yenu lakini ninyi si watu wa kupanga mikakati dhidi yao, adui anawashambulia na anawanyang’anya miji yenu mikononi mwenu alhali ninyi hamkasiriki!

Jicho la adui halilali kwa ajili ya kuwashambulia ninyi, lakini ninyi mko katika ghafla na kutojua, kushindwa ni kwa wale wanaoacha kusaidiana.

Naapa kwa Mwenyezi Mungu, nadhani kama vita vikipamba moto na joto la kifo likawafikia, mtafarakana na kuondoka kando ya mtoto wa Abu Talib kama vile kichwa kinavyotengana na mwili!

Naapa kwa Mwenyezi Mungu, mtu anayemwachia adui amtawale nafsi yake mpaka ale nyama yake, avunje mifupa yake na abandue ngozi yake, basi ulegevu wake ni mkubwa sana na moyo wake ni mdogo na dhaifu mno.”

Amirul Muuminina (amani iwe juu yake) mwishoni mwa maneno yake anasema:

“Ewe msikilizaji! Ikiwa wewe pia unataka kuwa katika unyonge na ulegevu kama mtu huyu, basi kuwa!

Lakini mimi naapa kwa Mwenyezi Mungu, sitakaa chini na kabla ya kumpa adui fursa, nitampiga pigo kubwa kwa upanga mkali juu ya mwili wake kiasi kwamba vipande vya mifupa ya kichwa chake vitaruka na mikono na hatua zake zitatengana, baada ya hapo, kitakuwa kile anachotaka Mwenyezi Mungu.

Enyi watu! Mimi nina haki juu yenu na ninyi mna haki juu yangu. Ama haki yenu juu yangu ni kwamba nisinyime nasaha zangu kwenu, na nitumie hazina yenu (Baitul-Maal) katika njia yenu, na niwafundishe ili mtokomeze ujinga na niwalee ili mujifunze. Na ama haki yangu juu yenu ni kwamba muwe waaminifu katika kiapo chenu cha utii kwangu, na msiache kutoa nasaha kwa dhahiri na kwa siri. Kila ninapowaita muitike, na kila ninapoamuru mtoe utii.” [1]

Chanzo

[1] Sehemu ya hotuba hii Tabari ameileta katika tarehe yake; Mustadrak wa Madarik Nahjul Balagha, ukurasa wa 242. Ibn Abil Hadid anasema: “Hotuba hii Imamu (amani iwe juu yake) aliitoa baada ya kumalizika kwa mambo ya Khawarij huko Nahrawan.” (Juzuu ya 2, ukurasa wa 192) Na baadhi wamesema: “Imamu (amani iwe juu yake) alitoa hotuba hii baada ya kurejea kutoka kwenye vita vya Khawarij na kulegalega kwa jeshi lake katika kujiandaa kupigana na watu wa Shamu.” (Na dhahiri ya hotuba hii inaunga mkono maoni haya) (Juzuu ya 2 ya Ibn Abil Hadid, ukurasa wa 194).